Tuesday 23 July 2013

FFU WAPINDUKA NA GARI NA MMOJA WAO KUFARIKI PAPO HAPO WAKATI WAKIELEKEA KWENYE ENEO LA TUKIO KUZUIA MAANDAMANO HUKO KILIMANJARO..!!

ASKARI mmoja wa Kikosi cha Kutuliza Ghasia (FFU) Mkoani Kilimanjaro, Fidelis Mwaliyatabu, amefariki dunia papo hapo na wengine tisa akiwamo Mkuu wa Kikosi hicho kujeruhiwa vibaya baada ya gari lao kupinduka katika kijiji cha Kilingi, wilaya ya Siha, wakati wakienda kuzima vurugu za wananchi.
Ajali hiyo ilitokea wakati kikosi hicho kikielekea katika kijiji cha Karansi kwa ajili ya kukabiliana na wananchi waliokuwa wakiandamana kupinga wenzao waliokamatwa usiku wa manane baada ya kuvamia mashamba mali ya Shirika la Roho Mtakatifu-Kilasara.
Taarifa kutoka kijijini humo zilieleza kwamba wanakijiji waliamua kuandamana baada ya wenzao watano kukamatwa na Jeshi la Polisi nyakati za usiku kwa mahojiano kutokana na kukabiliwa na tuhuma za kushawishi wanakijiji wenzao kuvamia maeneo ya Shule ya Kilasara na kusababisha hasara kubwa kwa shule hiyo.
Kufuatia kukamatwa kwa watuhumiwa hao, wanakijiji waliamua kuaandamana hadi katika kituo cha polisi ili kuwatoa wenzao hali ilisababisha jeshi hilo kutumia mabomu ya machozi kuwatawanya, jambo ambalo lilishindikana kutokana na wingi wa watu walikuwa wanaandamana.
Inadaiwa kuwa wananchi hao walijikusanya na walianza kuandamana kuanzia majira ya saa 7 usiku kuelekea kituo cha polisi ili kuwatoa wenzao walikuwa wanashikiliwa.
Wananchi wanaoshikiliwa na jeshi hilo ni John Sokoine, Abeli Solomoni, Christopher Solomon na aliyetambuliwa kwa jina moja tu la Julius. Wote walikamatwa usiku wa kuamkia jana.
Mnamo Juni 11, mwaka huu majira ya mchana wananchi wa kijiji hicho walivamia eneo lenye ukubwa wa hekta mbili na kufyeka mazao mbalimbali yaliyokuwa shambani hapo kwa madai kuwa wamiliki wa shule hiyo wamechukua eneo hilo kinyume cha taratibu.
Kwa upande wake, Mkuu wa Shirika la Roho Mtakatifu, Kanda ya Afrika, Padri Jerome Okama, aliushutumu uongozi wa kijiji hicho kwa kuvifumbia macho vitendo vya wananchi kujichukulia sheria mkononi wakati wakitambua kuwa eneo hilo lenye ukubwa wa hekta 8.9 linamilikiwa na shirika hilo kihalali.
Kamanda wa Polisi mkoani hapa, Robert Boaz, akizungumza na NIPASHE kwa njia ya simu kutoka wilayani humo jana jioni, alisema askari hao walipata ajali hiyo majira ya saa 6.45 mchana katika kijiji cha Kilingi nje kidogo ya mji wa Sanya Juu.
Alisema askari hao wamelazwa katika Hospitali ya Rufaa ya KCMC na wengine wamelazwa katika Hospitali ya Taifa ya Ugonjwa wa Kifua Kikuu ya Kibong'oto ilioyopo wilayani Siha na kwamba watano kati yao hali zao ni mbaya.
Alitaja gari la Polisi lililopinduka na kuua kuwa ni Toyota Land Cruiser lenye namba PT 2070 lililokuwa likiendeshwa na Sajenti Herman Dancan. Chanzo cha ajali hiyo ni mwendo kasi na kuacha njia na kupinduka.
Aliwataja waliojeruhiwa katika ajali hiyo kuwa ni Mkuu wa FFU mkoani hapa, ASP Nonino, Renatus Misigalo, Alfonce Joseph, Koplo Elifuraha Lenare, Peter Albert, Bashiri Yusuph, George Mwakyusa na Gaspar Mwapunda.
Alisema mwili wa marehemu umehifadhiwa katika hospitali ya Kibong'oto.

WAJANE WA WANAJESHI WA JWTZ WALIOUAWA HUKO DARFUL WAILILIA SERIKALI....!!

WAJANE wa askari saba wa Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ), wameililia Serikali iwasaidie kuwajengea nyumba za kuishi, ili kuepuka matatizo ya kifamilia ambayo yanaweza kuwapata baada ya kufiwa. Mbali ya kuomba msaada huo, wajane hao pia wameiomba Serikali iwasaidie kusomesha watoto wao kutokana na uwezo kuwa mdogo. 


Wakizungumza kwa uchungu kwa nyakati tofauti jana, wakati wa kuaga miili saba ya askari hao, katika viwanja vya makao makuu ya JWTZ Upanga, Dar es Salaam, wajane hao wamesema wamebaki katika wakati mgumu wa kukabiliana na maisha.

Mmoja wa wajane hao, Mariam Masudi (30), ambaye aliolewa na marehemu Sajenti Shaibu Salehe Othman na kufanikiwa kuzaa naye watoto wanne, ambao ni Salma Shaibu ambaye anasoma kidato cha nne, Nadhira Shaibu (darasa la sita), Ilham Shaibu (darasa la pili) na Abdulhakim Shaibu (chekechea), akielezea masikitiko yake yakuondokewa na mume wake alisema:

Nina uchungu sana wa kuondokewa na mwenzangu, nilikuwa namtegemea mume wangu kwa kila kitu.

“Naomba jeshi, linisaidie kusomesha watoto wangu…tumesikia tutapewa fedha, lakini nakwambia nyumba ndiyo itakuwa sehemu ya kutuenzi na watoto wangu,” alisema huku akibubujikwa na machozi.


Naye, mjane Maria Reston (30), ambaye alikuwa ameolewa na Koplo Oswald Chaula alisema anaishi katika nyumba za jeshi katika kota za Chabuluma mkoani Ruvuma, ameachwa na watoto wanne.

Msiba huu, unaniuma sielewi mume wangu amekufaje jamani, kwa kuwa imetokea namwachia Mungu.

“Taarifa za vifo vya wanajeshi nilizipata kwenye magazeti, sijui kwanini nilihisi mume wangu atakuwa miongoni mwao.

“Niliposoma nikaona jina la mume wangu, siamini kama kweli mume wangu amefariki jamani,” alisema Maria kwa uchungu.


Aliwataja watoto wake, kuwa ni Elizabeth Chaula (anasoma kidato cha kwanza), Clares (darasa la sita), Eliud (darasa la kwanza) na Joshua (ana umri wa miezi 10).

MAFUTA YA UBUYU YAZUA MAPYA TENA....ALBINO WAKATAZWA KUYATUMIA KWAAJILI YA NGOZI ZAO..!!

BAADHI ya wagonjwa wa Saratani waliolazwa katika Taasisi ya Saratani Ocean Road mjini Dar es Salaam, wamebainika wanatumia mafuta ya ubuyu wakati yanadaiwa kusababisha saratani ya ini. Uchunguzi uliofanywa na MTANZANIA katika taasisi hiyo, umebaini wagonjwa wengi wanatumia mafuta hayo kwa usiri mkubwa. Katika hatua nyingine, Chama cha Albino Tanzania (TAS), kimewataka watu wenye ulemavu wa ngozi (albino), wanaotumia mafuta hayo kuacha mara moja, hadi hapo Serikali itakapotoa taarifa rasmi kuhusu matumizi ya mafuta hayo kwa ngozi ya albino.

Katika uchunguzi huo, imebainika baadhi ya albino hutumia mafuta hayo kwa kujipaka huku wengine wakiwa na vidonda kwenye ngozi zao.

Akizungumza na MTANZANIA, Katibu wa Chama hicho Taifa, Ziyada Nsembo alisema, TAS hakina elimu kuhusu bidhaa hiyo, hivyo wanaotumia wanaweza kuathiri ngozi zao zaidi.

Tunawataka albino wanaotumia mafuta haya waache mpaka Serikali itakapotoa tamko rasmi kuwa mafuta hayo hayana athari kwa ngozi ya albino.

“Ngozi ya albino ni nyepesi, ina uwezo mkubwa wa kupitisha kemikali ndani ya mwili, ikiwa hayafai kunywa basi kwetu hayafai hata kujipaka, maana wengine wana vidonda. 


“Tumeamua kutoa kauli hii kwa sababu kuna mafuta ambayo albino hatakiwi kupaka mchana, huwa hayana uwezo wa kukinga mionzi ya jua. 

Haya mafuta ya ubuyu tunaelezwa kuwa yanalainisha ngozi, hatujui kama yanakinga ya mionzi ya jua, hilo ndilo tatizo letu, tunashauri yasitumike hadi wataalamu wa masuala ya ngozi ya albino watufahamishe,” alisema Katibu huyo.

Mmoja wa albino ambaye ni kiongozi, alisema ameshawahi kutumia mafuta hayo.

Wapo albino wanaotumia haya mafuta, hata mimi ni mmoja wapo, ila sikujua kama yana madhara, kwa sasa nimeacha kutumia.”

WANAJESHI 7 WA JWTZ WALIPIGANA MASAA MAWILI WAKIJARIBU KUUNUSURU UHAI WAO HUKO DARFUL KABLA MAUTI HAIJAWAFIKA...!!


WANAJESHI saba wa Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ), waliouawa wakati wakilinda amani Darfur nchini Sudan, walipigana kwa saa mbili wakati wakijitetea kabla ya kufikwa na mauti.
Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi nchini, Jenerali Davis Mwamunyange, alisema hayo jana Dar es Salaam, wakati akitoa salamu za rambirambi, wakati wa kuaga askari hao waliouawa Julai 13.
Katika shughuli hiyo iliyofanyika Makao Makuu ya Jeshi la Wananchi (JWTZ), Rais Jakaya Kikwete aliongoza waombolezaji kuaga mashujaa hao ambapo pia Makamu wa Rais, Dk Mohammed Gharib Bilal na mawaziri mbalimbali walihudhuria.
“Kikundi hicho (askari wa JWTZ) kilikuwa kikitokea eneo la Abeche, kwenda Nation na kilipofika umbali wa kilometa 25, doria hiyo ilipunguza mwendo kutokana na utelezi wa matope yaliyosababishwa na mvua.

“Ghafla kikundi hicho kilishambuliwa na watu ambao hawakufahamika, wakitumia silaha nzito za kivita,” alisema Jenerali Mwamunyange.
Alisema ulikuwa ni mtego wa mashambulizi na kwa mujibu wa taratibu za operesheni hizo, doria hiyo haikuwa na silaha nzito, lakini ililazimika kujibu mapigano hayo hadi kikundi kingine cha askari wa JWTZ, kilipoitwa kuongeza nguvu kunasua wenzao katika mtego huo.
Jenerali Mwamunyange alisema wakati kikundi hicho kikinasuliwa, askari hao walipoteza maisha kwa ujasiri mkubwa na wengine 14 kujeruhiwa.
Alisema Tanzania imefikwa na msiba huo wa mashujaa, ikiwa imeshiriki kulinda amani Sudan tangu mwaka 2007, ambapo askari wake wamekuwa wakitekeleza majukumu yake kwa weledi wa hali ya juu, kwa kushirikiana na vikundi vingine na wenyeji katika maeneo ya operesheni.
Majina yao Awali Kaimu Msemaji wa JWTZ, Meja Joseph Masanja, alitaja majina ya mashujaa hao na mahali wanapokwenda kuzikwa, kuwa ni pamoja na Sajini Shaibu Othman (Zanzibar) na Koplo Osward Chaulo (Kilolo, Iringa). Wengine ni Koplo Mohammed Ally (Zanzibar), Koplo Mohammed Chukulizo (Kigoma), Praiveti Rodney Ndunguru (Songea), Praiveti Fortunatus Msofe (Tanga) na Praiveti Peter Werema (Tarime, Mara).
Rais Kikwete alisema mauaji ya wanajeshi hao, yalimshitua, kumhuzunisha na kumkasirisha na kujikuta akijihoji kwa nini watu wa Sudan waue Watanzania.
Alisema Watanzania hao walikwenda kuwasaidia kupata amani, utulivu, kunusuru maisha yao na kuwaondolea mazingira ya wasiwasi ili wafanye shughuli zao kwa tija.
Alisema tangu kuanza kwa shughuli za ulinzi wa amani Darfur, walinzi wa amani 41 kutoka mataifa mbalimbali wameuawa, na 55 kujeruhiwa na hakusita kuamini kuwa waliofanya tukio hilo ni wasiotaka amani Darfur.
“Idadi hii ni kubwa, inahitaji kutafakari vizuri na kutazama upya mfumo wa kiwango cha kujilinda kwa wanajeshi… lazima uwezo huo uongezwe ili kupunguza vifo zaidi,” alisema Rais Kikwete.
Aliahidi kufikisha maombi hayo kwa Umoja wa Afrika (AU) na Umoja wa Mataifa (UN), ili walitazame vizuri. Mchango wa Tanzania Rais Kikwete alisema Tanzania tangu Uhuru imekuwa ikijitolea kusaidia wanyonge dhidi ubaguzi, uonevu na wengine ambao njia za diplomasia zimekuwa zikitumika.
Aidha, alisema wakati wote walipoombwa, walijua uwezekano wa askari wao kujeruhiwa au kupoteza maisha, ni mambo yaliyofikiriwa kuwa yanaweza kutokea kwani walikwenda kwenye maeneo ya hatari, yenye mapigano.
Alisema kutokea hayo si ajabu, lakini hadhari kubwa ilichukuliwa kwa kupewa mafunzo, zana za kujihami, kujilinda na kutekeleza majukumu.
Rais Kikwete alisema baada ya mauaji hayo ya Darfur alizungumza na Katibu Mkuu wa UN, Ban Ki-moon ambaye alielezea masikitiko yake na kutoa pole nyingi, na kueleza kwamba alizungumza na Rais wa Sudan, Omar Al-Bashir, ili achukue hatua ya kusaka na kuwaadabisha wahalifu hao.
“Nami pia nilifanya mazungumzo na Rais wa Sudan, na alielezea masikitiko yake na nilimsisitizia umuhimu wa Serikali yake kufanya hivyo, kwa kuwa tukio hilo limetokea huko na hivyo waliofanya hivyo ni Wasudani,” alisema Rais Kikwete.
Alisema alimsisitiza, kwamba kwa kuwa mauaji hayo yamefanyika katika mamlaka ya Sudan, waliohusika wawe Waasia au Wasudani, lakini achukue hadhari zote kuwasaka.
Waziri Ulinzi Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Shamsi Vuai Nahodha, alisema Watanzania wamesikitishwa na mauaji hayo na inaweza kuwa mkakati wa kufifisha juhudi za UN kuleta amani.
“Wizara itatoa kila msaada kuwezesha maziko na kusaidia familia za marehemu na waliojeruhiwa,” alisema Nahodha.
Akitoa salamu za rambirambi kwa niaba ya Rais wa Zanzibar, Dk Ali Mohammed Shein, Meja Jenerali Salum Mustapha Kijuu, Kamanda wa Kikosi cha Nchi Kavu, alisema tukio hilo linasikitisha na ni msiba wa Taifa kwa kuwa askari hao walikufa kazini na ni mashujaa.
Katika eneo hilo, miili ya wanajeshi hao iliingia kila mmoja kwa gari maalumu la Jeshi na kupokewa na maofisa wa JWTZ na kupelekwa sehemu iliyoandaliwa kuagwa. UN itatoa medali kwa kila askari, kwa kutambua mchango wao.